Tuesday, February 7, 2012

JAJI AJITOA KESI YA LEMA


JAJI wa Mahakama Kuu, Aloyce Mujulizi  jana alijitoa kusikiliza kesi ya kupinga ushindi wa Mbunge wa Jimbo la Arusha mjini ,Godbless Lema (Chadema)  baada ya upande wa utetezi kuwasilisha notisi ya kutokuwa na imani naye kutokana na Kampuni ya Uwakili ya Imma aliyokuwa akifanya kazi , kutuhumiwa na ufisadi kwa kusaidia  kuchotwa fedha Benki Kuu (BOT) fedha ambazo zilidaiwa kusaidia ushindi wa CCM mwaka 2005.


Wakili wa Lema, Method Kimomogoro, aliwasilisha  notisi hiyo ya kuendelea kutokuwa na imani na jaji huyo Januari 31 mwaka huu na jana, aliendelea kusisitiza kuwa mteja wake (Lema) hana imani na Jaji huyo kwani chama chake cha Chadema kilishiriki kuituhumu kampuni ya Imma kwa kusaidia Kampuni ya Deep Green Ltd kuchota fedha BOT.



“Kwa kuwa maneno haya yalitamkwa na Chadema na yalitolewa pia bungeni na Kampuni ya Imma haikuwahi kukanusha kama ni kweli au la, mteja wangu anaamini, wewe  wakati huo ulikuwa mmoja ya wanahisa katika kampuni hiyo,  hivyo anahofu  hautamtendea haki katika kesi hii hivyo tunaomba kwa busara ujitoe,” alisema Kimomogoro.


Alisema mteja wake yupo tayari kutoa ushahidi juu ya kutuhumiwa kampuni ya Imma, kuhusika na ufisadi huo ambao ulielezwa  fedha zake hizo ndizo ambazo zilisaidia ushindi wa CCM mwaka 2005.


Jaji Mujulizi alitangaza uamuzi wa kujitoa baada ya mawakili wa pande zote kutoa hoja zao kwa zaidi ya saa mbili huku  wakili wa utetezi, Alute Mungwai, akieleza kupinga notisi hiyo ya kutokuwa na imani na jaji kwa maelezo imewasilishwa kinyume cha sheria, haina ukweli, imejaa majungu, inashusha heshma na hadhi ya mahakama na jaji huyo kwani tuhuma za Imma hazijathibitishwa

  
Jaji 
Akitoa uamuzi wake, Jaji Mujulizi alisema anachukua uamuzi wa kujitoa kwa kuzingatia heshima na maslahi ya haki hasa kutokana na mlalamikiwa kueleza kutokuwa na imani naye.

Jaji Mujulizi alisema amechukua uamuzi huo pia ili kuhakikisha kesi hiyo isiendelee kupigwa danadana na lazima ifike kikomo kwani ushahidi unaonyesha  upande wa walalamikiwa una lengo la kuchelewesha kesi hiyo.



Akinukuu kesi mbalimbali zilizowahi kufikiwa uamuzi kama huo, Jaji Mujulizi alisema  kimsingi shauri lililopo mbele yake linahusiana na kesi ya uchaguzi ambayo inapangiwa muda maalumu kumalizika na sasa imebaki miezi minne pekee kufikia mwisho.



“Notisi iliyowasilishwa kuwa hawana imani na mimi , imekiuka  kila aina ya utaratibu na ni dhahiri wanachokifanya ni kuchelewesha tu  usikilizaji wa kesi hii”, alisema Jaji Mujulizi.



Hata hivyo,  Jaji Mujulizi alitoa siku tano kwa Lema kuwasilisha mahakamani hapo na nakala kumpatia yeye ambapo pia alisema  maelezo ya  kutokuwa na imani naye, yanatilia shaka uwezo wake na mahakama hiyo, wanapaswa Chadema  kuleta mahakamani tuhuma hizo kuwa Kampuni ya Imma ilihusika na fedha za EPA ndani ya siku tano.



Alisema pia  chadema wanaweza kuchukua hatua za kikatiba kuwasilisha maombi rasmi kwa Rais Jakaya Kikwete aunde tume kuchunguza sakata hilo na pia kama yeye hastahili kukalia ofisi ya jaji na wafanye hivyo kwa kuzingatia Katiba.



“Hatuwezi kukaa kila mtu akae na kuchafua wengine kwa kurudia rudia  na hadi kuamini kuwa ni ukweli,” alisema Jaji Mujulizi.


Awali, Wakili Mungwai alitoa hoja mbali mbali za kisheria kupinga notisi ya kumtaka jaji huyo kutojitoa na kueleza kuwa kama akikubali kujitoa itaonyesha amekubali kuhusika na tuhuma za ufisadi na hivyo itaathiri heshima na  hadhi yake na mahakama kwa ujumla.




Lema atamba   

Mara baada ya uamuzi huo, nje ya Mahakama akizungumza na waandishi wa habari, Lema alisema ndani ya siku tano watawasilisha ushahidi wa tuhuma zao bila ya matatizo.

“Tuna ushahidi wa kutosha juu ya kampuni ya ImmaAdvocate  na hatuna shaka juu ya hili”, alisema Lema.


Wafuasi wachache wa Chadema ambao jana walifika mahakamani, walipokea uamuzi ya Jaji Mujulizi kwa shangwe na mmoja nusura ajikute akitiwa nguvuni baada ya kupiga makofi mahakamani mara baada ya jaji kusema anajitoa
Mwananchi. 

No comments: