Sunday, March 11, 2012


WAWATANGAZA MPONDA NKYA KUWA MAADUI NAMBA MOJA WA SEKTA YA  AFYA...


CHAMA cha Madaktari Tanzania (Mat) kimetangaza kusitisha mgomo wa nchi nzima kuanzia jana mchana, kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kumheshimu Rais Jakaya Kikwete, huku kikiwatangaza Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda na naibu wake, Dk Lucy Nkya kuwa maadui namba moja wa sekta ya afya nchini.

Uamuzi huo wa kurejea kazini umekuja siku nne tangu madaktari hao walipoanza mgomo kwa mara ya pili, wakishinikiza Serikali kutekeleza madai yao, likiwemo la Dk Mponda na Dk Nkya kujiuzulu.


Februari 9 mwaka huu madaktari hao walirejea kazini baada ya kugoma kwa siku 17 wakishinikiza Serikali itekeleze madai yao kadhaa, likiwemo suala la nyongeza ya posho na kuwajibishwa watendaji wakuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.


Kurejea kwao kazini kulikuja baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kutangaza kuwasimamisha kazi Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Blandina Nyoni na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa.


Taarifa ya viongozi wa MAT iliyotolewa mbele ya waandishi wa habari katika ukumbi wa Donbosco jijini Dar es Salaam, walisema wamemsimamisha uanachama Dk Nkya kwa kipindi cha miaka miwili na kuongeza kuwa licha ya madaktari kurejea kazini, hawako tayari kufanya kazi chini ya uongozi wa mawaziri hao.


Uamuzi kusitisha mgomo ulikuja baada ya viongozi wa Mat hicho na wale wa Jumuiya ya Madaktari kukutana na Rais Jakaya Kikwete Ikulu, juzi kujadili mgogoro wao.



Kabla ya kufikia uamuzi huo wa kusitisha mgomo wao ulioanza Jumatano iliyopita, kulikuwa na mvutano mkali kwenye kikao chao cha ndani kilichofanyika ukumbi wa Donbosco, kutokana na baadhi yao kuafiki kurejea kazini huku wengine wakitaka mgomo huo uendelee hadi hapo Dk Mponda na Dk Nkya watakapojiuzulu.



Ufafanuzi wa Mat


Rais wa Mat, Dk Namala Mkopi, alisema katika kikao chao na Rais Kikwete walimweleza jinsi mawaziri hao wasivyokuwa na uwezo wa kusimamia sekta nzima ya afya.


“Tulimweleza Rais kila kitu na yeye ametuelewa. Pia tulibaini kuwa kuna taarifa za uongo alizokuwa akipelekewa na baadhi ya watu,” alisema Dk Mkopi.


Alisema kuwa Rais Kikwete ameyapokea madai yao kwa uzito mkubwa na kuwaahidi kuwa atayashughulikia.


“Kutokana na hali hiyo leo (jana) tumefanya kikao cha ndani na madaktari na kuwaeleza yaliyojiri katika kikao chetu cha jana (juzi) na Rais Kikwete na wamekubali kurejea kazini, hivyo kuanzia sasa tumerejea kazini kama awali,” alisema Mkopi.


Alifafanua kuwa mgomo wao haukuwa mashindano baina yao na Serikali wala kuiumiza jamii, bali walikuwa wakitafuta suluhu ya kuboresha huduma za afya nchini na kwamba hatua waliyofikia sasa ni nzuri.


“Madaktari wote waliokuwa katika mgomo warejee kazini, na hivi sasa kutakuwa na mawasiliano ya karibu ili kuwaeleza hatua zilizofikiwa katika suala zima la Serikali kutekeleza madai yetu, tuna imani na Rais na tunajua atatekeleza madai yetu,” alisema Dk Mkopi.


Sharti kwa Rais


Dk Mkopi alisema kuwa katika mkutanoh huo walimweleza wazi Rais Kikwete, kuwa madaktari hawako tayari kufanya kazi na mawaziri wa afya.


Alisema kuwa Dk Mponda na naibu wake Dk Nkya ni maadui namba moja wa sekta ya afya na kwamba ili madai yao yaweze kutekelezwa na kufikia hatua wanayoitaka, mawaziri hao wanatakiwa wasiwepo tena katika wizara hiyo.


“Hatuna imani na mawaziri hao hata kidogo na hatuwezi kufanya kazi nao na  katika kikao chetu, madaktari wote wamekubaliana hivyo,” alisema Mkopi.


Alipoulizwa kama wamempa rais muda wa kutekeleze madai yao, alisema hawakumpangia, wala rais hakuwaeleza suala hilo atalishughulikia kwa kipindi gani, isipokuwa watakuwa wakipeana taarifa ya kila kitu kitakachokuwa kikiendelea.


Dk Nkya asimamishwa Mat


Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Rodrick Kabangila alisema kuwa MAT kimemsimamisha uanachama Dk Nkya kwa muda wa miaka miwili.


“Kwa  kipindi cha miaka miwili hatakuwa mwanachama hai wa Mat, tumeamua kumsimamisha uanachama kwa kuwa pamoja na mambo mengine, hatuna imani naye,” alisema Dk Kabangila.


Kabla ya maamuzi


Kabla ya kuzungumza na waandishi wa habari madaktari hao walikuwa na kikao cha ndani ambacho waandishi wa habari hawakuruhusiwa kuhudhuria.


Habari za ndani kutoka katika kikao hicho kilichoanza saa 4:50 asubuhi na kumalizika saa 6:53 mchana, zinaeleza kuwa madaktari hao walivutana kuhusu mgomo, ambapo baadhi yao walitaka uendelee huku wengine wakitaka usitishwe kuokoa maisha ya watu wanaokufa bila hatia.


Taarifa zinaeleza kuwa asilimia kubwa ya madaktari hao ilionyesha kuwa na imani na Rais Kikwete hali iliyowafanya wakubaliane kwa urahisi.


Kauli ya Dk Mponda


Gazeti hili lilipomtafuta Dk Mponda jana kwa simu, muda mfupi baada ya madaktari hao kusitisha mgomo wao; alisema kuwa hana la kuzngumza.


“Katika hilo sina maoni yoyote na wala siwezi kusema kitu chochote,” alisema Dk Mponda na kukata simu.


Rais alivyoingilia kati



Juzi Rais Kikwete aliahirisha kulihutubia Taifa kupitia wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam, badala yake akaitisha mkutano wa faragha na viongozi wa MAT.


Rais Kikwete alifanya kikao hicho juzi mchana Ikulu jijini Dar es Salaam, huku kukiwa na amri ya Mahakama ya Kazi inayowaamuru madaktari hao kurejea kazini kutokana na kesi iliyofunguliwa na Mwanasheria wa Serikali.


Mpaka madaktari hao wanakwenda kuonana na Rais Kikwete, walikuwa katika mgomo kwa maelezo kuwa hawana taarifa rasmi ya Mahakama.


Kikao cha juzi kilikuwa cha kwanza kwa Rais Kikwete kukutana na madaktari hao ambao kwa sasa wanagoma kwa mara ya pili.



Baada ya kikao chao na rais, madaktari walitoka Ikulu bila kuzungumzia chochote.


Katibu Mkuu wa Mat, Dk Kabangila alikataa kata kata kuzungumzia kilichoazimiwa kwenye mkutano huo na Rais Kikwete akasisitiza kuwa ataweka mambo hadharani siku inayofuata (jana).




Hali ilivyokuwa hospitali Dar


Ibrahim Yamola na Aidan Mhando wanaripoti kuwa kuanzia jana mchana huduma katika hospitali hizo, zilirejea katika hali ya kawaida baada ya madaktari kurejea kazini.


Katika hospitali za Mwananyamala, Amana na Temeke huduma zilikuwa zinatolewa ingawa kulikuwa na idadi ndogo ya wagonjwa kama ilivyo kawaida yake.

 “Nimefika kumleta mwanangu anaumwa malaria na nimetibiwa kama kawaida nafikiri mgomo wao umemalizika,” alisema Mohamed Yasin mkazi wa Kinondoni aliyekuwa katika hospitali ya Mwananyamala.


Chanzo cha mgogoro


Januari 23 mwaka huu, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Stephen Ulimboka alitangaza mgomo wa madaktari nchi nzima lengo likiwa  kuishinikiza Serikali kutekeleza madai yao.



Joto lilipanda zaidi baada ya kufukuzwa kwa madaktari waliokuwa kwenye mafunzo ya vitendo katika hosptali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) ambapo Mwenyekiti wa Mat, Deogratus, alisema wapo 225 huku Serikali kwa upande wake ikidai walikuwa 197.







MASHINE YA MATITI YAINGIA NCHINI 
 
WANAWAKE WAFURIKA KUPATA HUDUMA
Na Julieth Kulangwa
BIASHARA huria imezua mengi. Hali kadhalika Sayansi na Tekenolojia nayo, imeleta mengi. Katika kuwaondolea kero  wanawake wenye matiti yaliyosinyaa hapa nchini, wataalamu kutoka China wameanza kutoa huduma ya kunyanyua matiti hayo kwa kutumia mashine maalumu.
Wachina wamejipatia umaarufu katika kuleta bidhaa mbalimbali hapa nchini, zikiwamo za kuongeza nguvu za kiume, kupunguza uzito, kuotesha nywele, kujichubua (kumfanya mtu mweusi awe mweupe), kuongeza makalio nk.
Huduma hiyo ya kusimamisha matiti yaliyolala, imeanza kutolewa katika Saluni ya Blue Palace, iliyopo nyuma ya Shule ya Mapambano, Sinza jijini Dar es Salaam.
Haikuwa rahisi kuweza kuamini kuwa vitu kama hivi vinaweza kupatikana Tanzania. Mwananchi Jumapili lilifunga safari mpaka kwenye saluni hiyo inayomilikiwa na Sarafina Mtweve, kujionea jinsi teknolojia hiyo inavyofanya kazi.
Mbali na meneja wa saluni hiyo, Trust Mwembe, pia alikuwepo mtaalamu kutoka China aitwaye, Ciisy Pang, ni binti wa miaka 23 tu, lakini anasema kwa miaka minne amefanya kazi hiyo na kuwasaidia wanawake mbalimbali waliokuwa wakikerwa na matiti yaliyolegea au kuanguka.
Pang na kundi lake wanatoa huduma hii kwa gharama ya Sh150,000 kwa kuanzia, ingawa wanahisi gharama hizo zitapanda katika siku chache zijazo.
 Jinsi matiti yanavyosimamishwa
Mashine hiyo inayoitwa ‘Beauty Machine’ ina uwezo wa kusimamisha matiti ya kila saizi kwa kuwa huambatanishwa na vibakuli (cups) kama unavyoona pichani.
Kazi kubwa ya mashine hiyo ni kuamsha misuli ambayo hushikilia nyama za matiti.
Pang anasema, zoezi la kusimamisha matiti huchukua wiki tatu mpaka sita, inategemea aina ya mteja na wakati mwingine juhudi zake.
Mtaalamu huyo ambaye anazungumza Kichina na kutafsiriwa na meneja wa saluni hiyo, anaelezea namna anavyofanya kazi ya kuyarudisha matiti  kwa muda huo.
 “Kwanza unapaswa ujue kuwa hatutumii dawa yoyote katika zoezi hili, mteja wetu akifika hapa, kinachotumika ni mashine tu ambayo hutumia umeme kama zilivyo dryer  za nywele,
“Baada ya kumlaza katika kitanda kile, tunachukua kitu mfano wa bakuli (cups) mbili kulingana na ukubwa wa matiti yake, tunayatumbukiza humo, kisha tunawasha mashine,” anasema Pang.
Mtaalamu huyo anasema mashine hiyo ikiwashwa  inavuta kama ‘vacuum’, na inaweza kuongezwa kasi au kupunguzwa kama inavyofanyika kwenye mashine za kufanyia mazoezi.
“Tunaiwasha mashine kwa muda wa dakika 45, mteja atachagua siku mbili katika wiki za kufanya zoezi hili mpaka litakapokamilika,”anasema Pang.
Tangu mashine hiyo iwasili nchini, takribani mwezi mmoja uliopita, Pang anasema ana wateja wanane anaowahudumia kwa nyakati tofauti ambao wamekiri kuwa maendeleo yanatia moyo.
 Ni kweli mashine hii inasaidia?
 Akizungumza kwa njia ya simu, mmoja wa wateja anayepata huduma hiyo ambaye alijitambulisha kwa jina moja tu Irene anasema, ni wiki ya tatu sasa tangu aanze kupata huduma hiyo, anakiri kuwa matiti yake sasa yameanza kuwa magumu tofauti na mwanzo.
 “Kusema kweli nilikuwa na matiti yaliyosinyaa wala si kulala tu kama ulivyouliza, ila naona sasa yameanza kuwa magumu na kurudi juu kidogo,” anasema Irene.
 Akizungumzia ugumu anaoupata katika zoezi hilo, anasema safari za kila wiki saluni na zile dakika 45 za kukaa kwenye mashine zinamchosha, lakini kwa kuwa amedhamiria, amejitoa mpaka zoezi hilo litakapokamilika.
Matiti yanaweza kulegea tena?
Pang anasema kama matiti yanalegea kwa sababu fulani mfano uzazi wa watoto wengi, basi yanaweza kulegea tena kama mtu atajifungua na kunyonyesha kwa muda huo.Aidha anasema wanawake wenye matiti makubwa, ni rahisi kuanguka kama hawatayavalisha sidiria kwa muda mrefu.
 “Wanawake wenye matiti makubwa huwa nawashauri kuvaa sidiria hasa wakati wa mchana na usiku wanaweza kuacha kuzivaa, hii inasaidia kuimarisha misuli inayoyabeba matiti,” anasema Pang.
 Jamii inazungumziaje jambo hili
Baada ya kusikia kuwepo kwa mashine hii nchini, wanawake mbalimbali wamesema wanatamani kupata huduma hiyo lakini wengine, walionyesha woga juu ya matokeo yake.
 “Ni kweli baada ya kunyonyesha watoto wawili sasa matiti yamelegea kabisa, natamani yarudi kama wakati ule wa usichana wangu, lakini nahofia huenda mbele ya safari nikapata madhara,” anasema Linda Masatu.
Linda anaongeza kusema kuwa ni vizuri mwanamke akawa na matiti yaliyojaa vizuri, lakini anahofia njia zinaweza kuwa na madhara, huku akisema kama ingetokea njia nyingine ya asili asingesita kuifuata.
Naye Batuli Famau, anasema mwanamke anapokuwa na matiti yaliyosinyaa mvuto wake hupungua, hata anapovaa sidiria anakuwa amebadili mwonekano wa nje tu, lakini ndani bado anakuwa vilevile.
“Mwanamke mrembo ni yule mwenye matiti mazuri, sasa inapobidi kutumia njia fulani ili yarudi kama tulipokuwa vigoli, tutafanya tu ili mradi kama njia hizo hazitatuangamiza,” anasema
Wanaume nao wameonekana kuunga mkono zoezi la kusimamisha matiti ingawa wengine hawaungi mkono utumiaji wa mashine hii.
Augustino Magara anasema: “Ni kweli mwanamke mwenye matiti magumu anavutia kuliko yaliolegea na kulala, lakini sasa tuwe makini kabla wake zetu hawajaumia katika mashine, hizi”
 “Wote tunajua sababu zilizosababisha matiti ya wake zetu yalegee, sioni sababu ya kusema tunataka yaliyomagumu, tuwapende wake zetu hivi hivi na tuwape moyo,” anasema Nganara.
Dk Innocent Mosha wa Kitengo cha Patholojia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, anasema ni vigumu kwa wataalamu wa afya kugundua madhara ya mashine hizo kwa haraka hadi pale uchunguzi utakapofanyika.
“Ingelikuwa mazoezi hayo yanachukua muda mfupi, kweli tungepata wasiwasi kwa kuwa, unapoisimamisha misuli kwa haraka ni lazima madhara yatokee, lakini hili la mazoezi, bado sifahamu,” anasema  Dk Mosha.

 

No comments: